1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUfaransa

Ufaransa yakumbwa na wimbi jipya la migomo

31 Januari 2023

Wafanyakazi wanaogoma nchini Ufaransa wamevuruga shughuli za kiuchumi na ratiba za shule katika siku ya pili ya maandamano ya nchi nzima kupinga mpango wa rais Emmanuel Macron kuongeza umri wa kustaafu.

https://p.dw.com/p/4MvCU
Frankreich | Landesweite Streiks gegen geplante Rentenreform
Picha: Lionel Urman/ABACA/picture alliance

Makundi ya watu yameandamana katika miji kote nchini Ufaransa kupinga mageuzi yanayopandisha umri wa kustafu kwa miaka miwili hadi 64, na ambayo yanatazamwa kama mtihani kwa uwezo wa Macron kupitisha mabadiliko wakati huu ambapo chama chake kimepoteza wingi wake bungeni. Vikitiwa msukumo na mafanikio yake mapema mwezi huu ambapo zaidi ya watu milioni moja waliingia mitaani, vyama vya wafanyakazi ambavyo vimekuwa vikipambana kudumisha nguvu na ushawishi wao viliuhimiza umma kujitokeza kwa wingi. Kura za maoni ya wananchi zinaonyesha idadi kubwa ya Wafaransa wanapinga mageuzi hayo, lakini Macron anakusudia kushikilia msimamo wake. Hapo jana rais huyo alisema mageuzi hayo ni muhimu ili kuhakikisha ufanyaji kazi wa mfumo wa pensheni.