1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUfaransa

Macron akabiliwa na maandamano zaidi ya sheria ya pensheni

Sylvia Mwehozi
17 Machi 2023

Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron amezidi kukabiliwa na shinikizo la maandamano na hoja ya kutokuwa na imani naye bungeni baada ya kupitisha mpango wa mageuzi tata ya pensheni bila ya kupigiwa kura katika bunge la taifa.

https://p.dw.com/p/4OqZ8
Frankreich Protest gegen Rentenreform
Picha: Aurelien Morissard/AP Photo/picture alliance

Maandamano makubwa yamezuka tena siku ya Ijumaa dhidi ya mpango wa serikali wa mageuzi ya pensheni uliogubikwa na utata, siku moja baada ya Rais Macron kulazimisha mpango huo kupitia bunge la baraza la seneti bila ya kura ya mwisho katika bunge la taifa.

Waziri Mkuu wa Ufaransa Elisabeth Borne siku ya Alhamisi alitumia kifungu cha 49.3 cha katiba kupitisha sheria ya mageuzi ya penshenikwa amri bila ya kura ya bunge la taifa na hatua hiyo imezua tafrani bungeni na uwasilishaji wa hoja ya kutokuwa na imani na serikali. Hali hiyo inampa Macron moja ya changamoto kubwa chini ya mwaka mmoja katika kipindi chake muhula wa pili na wa mwisho.

Ghasia zilizuka alhamis jioni mjini Paris wakati polisi walipotumia maji ya kuwasha na gesi ya kutoa machozi kutawanya waandamanaji wapatao 6,000 ambao walikusanyika katika eneo linalotizamana na bunge la kitaifa kupinga mageuzi hayo ya pensheni. Polisi mjini Paris ilisema kwamba imewakamata watu zaidi ya 200. Mapema siku ya Ijumaa, usafiri wa umma katikati mwa Paris ulikuwa umetatizika kwa muda baada ya wito wa hatua zaidi kutoka chama cha wafanyakazi cha CGT.

Frankreich Paris | Parlament zu Rentenreform
Bunge la baraza la seneti la Ufaransa lililoidhinisha sheria ya mageuzi ya pensheniPicha: PASCAL ROSSIGNOL/REUTERS

Katika miji mingine kama ya Rennes na Brest, waandamanaji walizuia kwa muda barabara, huku miji mingine ya Ufaransa ikishuhudia maandamano alhamis jioni. Shule na vyuo vikuu navyo vilizuiwa kwa sehemu fulani na waandamanaji vijana. Baadhi ya viwanda vimetangaza mgomo mpya au kurefusha mgomo, ingawa usambazaji wa petroli katika vituo vya mafuta hakujatatizika.

Bunge la Seneti Ufaransa laidhinisha mageuzi ya mfumo wa pensheniVyama vya wafanyakazi vilivyopanga migomo na maandamano dhidi mageuzi hayo vimeitisha maandamano zaidi wiki ijayo na vimeitaja hatua ya serikali kama "ya kukataa kabisa demokrasia".Bunge la Seneti Ufaransa laidhinisha mageuzi ya mfumo wa pensheni

Macron alitangaza mageuzi ya pensheni, ambayo yanajaribu kuongeza idadi ya miaka ambayo watu wanapaswa kufanya kazi ili kupokea pensheni kamili, katikati mwa kampeni yake ya kuchaguliwa tena mwaka jana. Umri wa kustaafu unaopendekezwa ni kutoka miaka 62 hadi 64.