1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaTunisia

Tunisia yajiandaa kwa uchaguzi

4 Oktoba 2024

Watunisia Jumapili wanapiga kura katika uchaguzi wa rais huku Rais wa sasa Kais Saied akionekana hana changamoto kubwa katika kuwania muhula wa pili, licha ya kukosolewa vikali katika uongozi wake wa miaka mitano.

https://p.dw.com/p/4lQdr
Uchaguzi- Tunisia
Halmashauri ya uchaguzi ya Tunisia, ISIE, imejiandaa kwa uchaguzi wa Oktoba 6. Picha ya maktaba, mpiga kura wakati wa uchaguzi wa duru ya pili ya uchaguzi wa wabunge Januari 2023.Picha: Hasan Mrad/Zuma/picture alliance

Uchaguzi wa rais wa Oktoba 6 katika taifa hilo la Kaskazini mwa Afrika ni wa tatu tangu maandamano yaliyosababisha kung'olewa madarakani kwa Rais Zine El Abidine Ben Ali mwaka 2011, mbabe wa kwanza aliyepinduliwa katika ghasia za vuguvugu la kiarabu ambalo pia liilisababisha mapinduzi kwa viongozi wa Misri, Libya na Yemen.

Waangalizi wa kimataifa walisifu maandamano yaliyofanywa awali mara mbili kwamba yalifuata kanuni za kidemokrasia. Lakini, safu ya kukamatwa na hatua zilizochukuliwa na Halmashauri ya kusimamia uchaguzi iliyoteuliwa na Saied imeibua maswali kuhusu iwapo uchaguzi wa mwaka huu utakuwa huru na wa haki. Vyama vya upinzani vinatoa wito kwa wananchi kuususia.

Rais wa zamani wa Tunisia | Zain Al Abidin ben Ali
Aliondolewa madarakani na vuguvugu la kiarabuPicha: Ammar Abd Rabbo/picture alliance/abaca

Tunisia ilisifiwa kama mafanikio ya pekee ya shinikizo la vuguvugu la kiarabu. Huku mapinduzi, mapambano ya kupinga mapinduzi na vita vya wenyewe kwa wenyewe vikiivuruga serikali mbalimbali katika eneo hilo, taifa hilo la Afrika Kaskazini lilikumbatia katiba mpya ya demokrasia na kushuhudia mashirika yake makuu ya kiraia kushinda Tuzo ya Amani ya Nobel kwa kufakinikisha kufikiwa kwa maelewano ya kisiasa.

Soma pia: Mgombea urais Tunisia ahukumiwa miaka 12 jela

Lakini viongozi wake wapya hawakuweza kuinua uchumi uliokuwa unasuasua na walighubikwa na malumbano ya kisiasa na matukio ya vurugu na ugaidi.

Licha ya hali hiyo, Saied, wakati huo akiwa na umri wa miaka 61 na ambaye hakuwa amejishughulisha sana na siasa, alishinda muhula wa kwanza mwaka wa 2019 akiahidi kuanzisha "Tunisia Mpya" na kukabidhi nguvu zaidi kwa vijana na serikali za mitaa.

Uchaguzi wa mwaka huu utatoa nafasi katika maoni ya watu wengi kuhusu mwelekeo ambao demokrasia inayofifia ya Tunisia imechukua tangu Saied alipiongia madarakani.

Wafuasi wake wanaonekana kuwa waaminifu kwake na ahadi ya kubadilisha Tunisia. Lakini Saied hana mafungamano na

chama chochote cha siasa, na haijulikani jinsi uungwaji mkono wake ulivyo miongoni mwa Watunisia.

Changamoto mpya kwa Saeid

Mgombea urais wa Tunisia I Kais Saied - Tunis
Kais Saied rais wa Tunisia anayegombea muhula wa pili.Picha: Fauque Nicolas/Images de Tunisie/ABACA/picture alliance

Ni kinyanganyiro cha kwanza cha urais tangu Saied alipobadilisha siasa za taifa hilo Julai 2021, kwa kutangaza hali ya hatari, kumfukuza kazi waziri mkuu, kusimamisha bunge na kuandika upya katiba ya Tunisia inayompa mamlaka zaidi.

Vitendo hivyo vilikasirisha vikundi vinavyounga mkono demokrasia na viongozi wa upinzani, na kuitaja hatua hiyo kama  mapinduzi. Lakini, licha ya hasira kutoka wanasiasa, wapiga kura waliidhinisha katiba mpya ya Saied katika kura ya maoni ingawa watu waliojitokeza walikuwa wachache.

Soma pia: Rais wa Tunisia amfuta kazi waziri mkuu

Mamlaka baadaye ilianza kuwakamata wakosoaji wa Saied wakiwemo waandishi wa habari, wanasheria, wanasiasa na watu wa mashirika ya kiraia, wakihukumiwa kwa kuhatarisha usalama wa nchi na kukiuka sheria dhidi ya habari ghushi ambayo waangalizi wanahoji kwamba inakandamiza upinzani.

Wagombea waambulia patupu

Maandamano- Tunisia
Maandamano ya Tunisia - Muandamanaji akiinua bango wakati wa maandamano dhidi ya Rais Kais Saied huko mjini Tunis.Picha: Hassene Dridi/AP Photo/picture alliance

Katika uchaguzi wa Oktoba 6 wengi walitaka kumpa changamoto Saied, lakini wachache walifanikiwa kufikia vigezo.

Wagombea kumi na saba waliotarajiwa waliwasilisha makaratasi ya kugombea,  halmashauri ya kusimamia uchaguzi ya Tunisia iliwaidhinisha watatu pekee,  Zouhair Maghzaoui, Ayachi Zammel na Kais Saied.

Maghzaoui ni mwanasiasa mkongwe ambaye amefanya kampeni dhidi ya mpango wa kiuchumi na kamatakama za kisiasa katika utawala wa Saied. Zammel ni mfanyabiashara anayeungwa mkono na wanasiasa uchaguzi. Wakati wa kampeni, alihukumiwa kifungo cha jela kwa kesi nne za ulaghai wa wapigakura zinazohusiana na sahihi ambazo timu yake ilikusanya kufuzu kuwania urais.

Soma pia: Umoja wa Mataifa walaani kukamatwa wanasheria Tunisia

Wengine waliokuwa na matumaini ya kushiriki walizuiwa na Halmashauri ya uchaguzi, ISIE, mwezi uliopita ilitupilia mbali uamuzi wa mahakama ulioamuru kuongeza wapinzani watatu wa ziada kwenye kinyangayiro cha urais. Wengi wakikamatwa, kuzuiliwa au kuhukumiwa kwa tuhuma zinazohusiana na shughuli za kisiasa.