1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Serikali ya Tanzania yatajwa kwenda kinyume na iliyopita

19 Novemba 2021

Nchini Tanzania mambo yanaonekana kwenda kasi zaidi baada ya serikali nchini humo kujitokeza hadharani na kuonyesha kwenda kinyume na aliyekuwa Rais wa awamu ya tano, hayati John Pombe Magufuli katika baadhi ya mambo.

https://p.dw.com/p/43G0c
Tansania Hafen von Tanga
Picha: picture alliance/Zandbergen-McP/Bildagentur-onlin

Miongoni mwa mambo ambayo  yanaweka wazi tofauti hiyo ni pamoja na mkataba wa ujenzi wa bandari ya Bagamoyo iliyoelezwa kuwa na mashariti magumu kama ilivyoelezwa hapo awali. Akizungumza na waandishi habari kuhusiana na mradi wa ujenzi wa bandari mpya ya Bagamoyo, Waziri wa nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Uwekezaji Godfrey Mwambe alisema kuwa hakuna mahali popote panapoonyesha kuwepo na masharti magumu katika ujenzi wa mradi huo.

Hatua hiyo ya serikali ya Tanzania kujitokeza hadharani kupitia Waziri Mwambe kuzungumza na waandishi habari hivi karibuni ya kwamba hakuna mahali popote panapoonyesha wawekezaji katika mradi huo wamepinga uendelezaji wa bandari yoyote zaidi ya mradi huo mpya, imezua mjadala katika mitandao ya kijamii huku ikiwaibua wachambuzi wa masuala ya kisiasa na watu mbalimbali kuhoji kuhusiana na sakata hilo.

Wachambuzi wahoji umakini wa wanaopewa dhamana ya kusimamia mambo

Tansania Geoffrey Mwambe
Waziri wa nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Uwekezaji Godfrey MwambePicha: TIC

Malesa Musa raia wa taifa hilo anashangazwa na serikali hiyohiyo kupingana na katika baadhi ya  mambo akisema jambo hilo linawachanganya wananchi na hivyo kushauri mambo yaweke wazi kama mkataba ulifikia hatua ya kusaini au hakusainiwa. Hali hii inaelezwa kuleta mashaka miongoni mwa Watanzaniakama anavyosema Dakta Donald Kasongi mchambuzi wa masuala ya kisiasa na kijamii nchini Tanzania anasema hali hiyo inaonesha mahaka ya umakini ya wale wanaopewa dhamana ya kusimamia mambo nchini humo.

Katika miaka ya nyuma wakati wa uhai wake aliyekuwa rais wa awamu ya tano hayati John Pombe Magufuli aliueleza umma kuwa mkataba wa ujenzi wa mradi wa bandari ya Bagamoyo ni mkataba wenye masharti magumu na kwamba ni kichaa peke yake anaweza kuingia mkataba huo.

Mwezi Oktoba mwaka 2015, ujenzi wa mradi wa Bagamoyo chini ya Ukanda Maalumu wa Kiuchumi wa Bagamoyo, SEZ ulizinduliwa rasmi na Rais wa awamu ya nne wa Tanzania Dokta Jakaya Mrisho Kikwete huku kukielezwa kuwa kukamilika kwa mradi huo utafungua fursa nyingi za kiuchumi kwa Watanzania.

DW: Dodoma