1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ramaphosa kutoa ushahidi dhidi ya Zuma

24 Machi 2021

Rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa atatowa ushahidi katika jopo la uchunguzi wa kesi ya muda mrefu ya  kadhia ya rushwa inayomuandama mtangulizi wake Jacob Zuma.

https://p.dw.com/p/3r3nv
Südafrika Präsident Jacob Zuma & Vize-Präsident Cyril Ramaphosa
Picha: Reuters/GCIS

Ramaphosa atatowa ushahidi wake kwa siku nne mwishoni mwa mwezi ujao kwa mujibu wa ofisi ya rais iliyotowa taarifa hiyo.

Jopo hilo linaongozwa na naibu jaji mkuu Raymond Zondo na liliundwa kuchunguza madai kwamba rais wa zamani Jacob Zuma aliwaruhusu wafanyabishara watatu waliokuwa karibu nae kufuja mali za serikali na kuwa na ushawishi katika hatua za kuwateua viongozi wa serikali wakati alipokuwa madarakani.

soma zaidi: Zuma asema hana hatia katika tuhuma za rushwa

Ramaphosa anatarajiwa kutoa ushahidi katika nafasi yake kama rais na kama makamu wa zamani wa rais wa nchi hiyo, na pia kama mwenyekiti na naibu mwenyekiti wa chama cha ANC.

Katika nyakati zote hizo alizokuwa naibu, Ramaphosa alikuwa chini ya uongozi wa Zuma. Mara kadhaa rais huyo wa Afrika Kusini amekuwa akisema kuna haja ya katiba na utawala wa sheria kuheshimiwa.

Zuma anakabiliwa na uwezekano wa kukamatwa baada ya kukataa kutii amri ya mahakama ya kumtaka afike kwenye jopo hilo la uchunguzi.Zuma anadai Zondo anaendesha uchunguzi kiuonevu.