1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaNamibia

Namibia yamzika rais wa zamani, Geingob

24 Februari 2024

Namibia imefanya mazishi ya kitaifa hii leo ya aliyekuwa rais wa nchi hiyo Hage Geingob, ambaye alifariki dunia mwanzoni mwa mwezi huu akiwa na umri wa miaka 82.

https://p.dw.com/p/4cq45
New York 2023 | Rais wa Namibia Hage Geingob
Rais wa zamani wa Namibia Hage Geingob amezikwa kitaifa na atakumbukwa kwa juhudi zake za kupambania uhuru wa NamibiaPicha: Caitlin Ochs/REUTERS

Shughuli ya mazishi ya kitaifa imefanyika kwenye uwanja wa michezo katikati mwa mji mkuu wa taifa hilo la kusini mwa Afrika, Windhoek na kuhudhuriwa na viongozi wengi wa mataifa ya bara hilo.

Rais Samia Suluhu Hassan wa Tanzania, William Ruto wa Kenya na Evarist Ndayishimiye wa Burundi ni miongoni mwa viongozi walioshiriki mazishi hayo.

Geingob, mmoja wa maveterani wa harakati za kupigania uhuru wa Namibia na waziri mkuu wa muda mrefu wa Namibia huru, aliaga dunia mnamo Februari 4 wiki chache baada ya kutangazwa kwamba amepata saratani.

Wengi wamemtaja kuwa kiongozi mahiri aliyepigania uhuru na ustawi wa Namibia katika kipindi chote cha maisha yake.

Muda mfupi baada ya kifo chache makamu wa rais Nangolo Mbumba aliapishwa kuwa rais mpya wa Namibia.