1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaAfrika Kusini

Rais Ramaphosa akabiliwa na shinikizo la kujiuzulu

1 Desemba 2022

Rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa amekuwa akikabiliwa leo na wito wa kujiuzulu baada uchunguzi wa bunge kubaini kuwa huenda alikiuka sheria za nchi.

https://p.dw.com/p/4KM3G
 Cyril Ramaphosa visits Rishi Sunak in London
Picha: Alberto Pezzali/AP/picture alliance

Rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa amekuwa akikabiliwa leo na wito wa kujiuzulu baada uchunguzi wa bunge kubaini kuwa huenda alikiuka sheria za nchi dhidi ya ufisadi kuhusiana na madai ya wizi wa kiasi kikubwa cha fedha katika shamba lake la Phala Phala game.

Wito huo umetolewa na wapinzani wake wa ndani katika Chama tawala ANC.

Wito huo unafuatia madai ya aliyekuwa mkuu wa idara ya ujasusi nchini humo Arthur Fraser, kwamba Ramaphosa alijaribu kuficha wizi wa pesa nyingi uliyotokea katika shamba lake mnamo mwaka 2020.

Kulingana na ripoti hiyo, Ramaphosa alidai pesa zilizoibwa zilikuwa Dola 580 000, na kupinga kiasi cha awali cha Dola milioni 4 milioni ambazo Fraser anadai ndizo zilizoporwa.

Rais Ramaphosa amekuwa akikana kufanya makosa yoyote akisisitiza kuwa hana uhusiano wowote na pesa iliyopatikana kwenye shamba lake.

Kamati kuu ya kitaifa ya chama cha ANC, ambayo ni ya juu zaidi ya kuchukua maamuzi, inatarajiwa kukutana kwa dharura leo jioni.