1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Olimpiki ya Tokyo mwaka 2020 huenda ikafanyika 2021

Deo Kaji Makomba
23 Machi 2020

Mashindano ya Olimpiki ya Japan yanatarajiwa kufanyika lakini uhakika wa kufanyika kwa mashindano hayo ni mwaka 2021 tofauti na miezi ijayo kama ilivyokuwa imepangwa hapo awali.

https://p.dw.com/p/3ZvHB
IOC-Präsident Thomas Bach
Rais wa Kamati ya Olimpiki ya kimataifa Thomas BachPicha: picture-alliance/dpa/KEYSTONE/J.C. Bott

Hatua hii imekuja mara baada ya Kamati ya kimataifa ya Olimpiki, IOC, Jumapili (22.03.2020) kutangaza ya kwamba ilikuwa ikifikiria kuahirisha mashindano hayo. Mataifa makubwa yanayoshiriki katika mashindano hayo kama vile Canada na Australia yaliongeza shinikizo kwa kusema kuwa hayatakwenda kushiriki mashindano ya Olimpiki mjini Tokyo kama mashindano hayo yatafanyika mwaka huu.

Rais wa Kamati ya Kimataifa ya Olimpiki, Thomas Bach, alituma barua kwa wanariadha akielezea maamuzi hayo na kwa nini inaweza kuchukua muda mrefu kiasi hicho wakati pia akikiri dhahiri shahiri ya kwamba kusogezwa mbele kwa ratiba ya sasa inaweza kuwa maarufu.

"Ninatambua kwamba hali hii isiyo ya kawaida inawaacha wengi wenu kuwa na maswali," ameandika rais katika barua yake na kuongeza kuwa." Natambua pia kwamba njia hii ya kimantiki inaweza kuwa haiendani na hisia ambazo wengi wenu mnatakiwa kuendana nazo.

Mwenendo wa IOC ulionekana hauwezi kuepukika kwa wiki kadhaa na shinikizo likizidi kupanda juu kutoka kwa robo yote ya wanariadha, wadhamini, watangazaji na zaidi ya kamati 200 za kitaifa za Olimpiki na mashirikisho ya michezo ya kimataifa.

Muda mfupi baada ya taarifa ya Bach, Kamati ya mashindano ya Olimpiki nchini Canada ilisema kuwa haitatuma timu zake katika mashindano hayo isipokuwa mashindano hayo endapo yataahirishwa kwa muda wa mwaka. Nchi ya Australia ilitoa taarifa yake huku ikisema kuwa iliwashauri wanamichezo wake kujiandaa kwa ajili ya mashindano ya Olimpiki mwaka 2021.

Bodi ya kamati kuu ya utendaji ya Olimpiki nchini Australia ilikubali kwa pamoja kwamba "timu ya Australia haikuweza kukusanyika nyumbani na nje ya nchi."

Kufanyika kwa Olimpiki ya Tokyo mwaka  2020 haiwezekani

Rais wa chama cha wanariadha duniani, Seb Coe, alituma barua kwa Rais wa Kamati ya Kimataifa ya Olimpiki, Thomas Bach, huku akisema kuwa kufanyika kwa mashindano hayo ya Olimpiki mwezi Julai haiwezekani wala haihitajiki." Aliorodhesha sababu lukuki ikiwemo ushindani usio sawa miongoni mwa wanariadha.

Kamati ya mashindano ya Olimpiki nchini Brazil na Slovenia ilitaka pia kuahirishwa kwa mashindano hayo hadi mwaka 2021. Bodi ya Olimpiki nchini Norway ilisema kuwa haitaki kuona wanariadha wake wakielekea mjini Tokyo hadi pale janga la kimataifa la virusi vya Corona litakapodhibitiwa.

Bodi ya uongozi na ufuatiliaji wa chama cha waogeleaji nchini Marekani na timu mbili za michezo mitatu ya juu ya msimu wa kiangazi wa majira ya joto waliitaka kamati yao ya kitaifa ya Olimpiki kuahirisha mashindano hayo.

Wanasiasa nchini Japan Jumatatu tarehe 23.03.2020 walikwamishwa na hatua iliyochukuliwa na Bach kutangaza kusogezwa mbele kwa mashindano hayo. 

Waziri mkuu wa Japan Shinzo Abe, akizungumza katika kikao cha bunge, alisema kuwa kuahirishwa kwa mashindano ya Olimpiki ya mjini Tokyo hayaepukiki endapo michezo hiyo haiwezi kuandaliwa kikamilifu kwa sababu ya kuwepo kwa janga la kimataifa la virusi vya Corona.

China Ostasien-Gipfel
Waziri mkuu wa Japan, Shinzo Abe.Picha: picture-alliance/AP/Wang Zhao

"Kama ni vigumu kuandaa michezo kwa uhakika, maamuzi ya kuahirisha mashindano hayo hayaepukiki," alisema Abe.

Abe alisema kuwa, tumaini lake IOC itafanya maamuzi mapema kama itakuwa imeahirisha mashindano hayo, kwa sababu mchakato huo unahusisha kazi nyingi na inatakiwa kuanza haraka iwezekanavyo.

Gavana wa mji wa Tokyo, Yurko Koike, aliunga mkono kauli ya Abe.

"IOC wanatakiwa kuchunguza kwa kina nini cha kufanya kuelekea wiki nne zijazo, na katika mchakato huo neno kuahirisha linaweza kujumuishwa." Alisema Koike.

Serikali ya Japani imetumia dola bilioni 12.6 kwa ajili ya kuandaa mashindano hayo ya Olimpiki, lakini taasisi ya ukaguzi ya taifa imeweka takwimu kwa zaidi ya mara mbili ya kiasi hicho. Kuna uwezekano wa kuongezeka kwa gharama kutokana na kuahirishwa kwa mashindano hayo na idadi kubwa ya matumizi kutoka katika hazina ya umma.

IOC ina mfuko wa hifadhi wa takribani dola bilioni 2 kwa ajili ya kujiendesha yenyewe na pia inayo bima itakayolipia gharama zote endapo kama mashindano hayo yakiahirishwa au kufutwa.

"Umma unatarajia na utasaidia kuahirishwa kwa mashindano hayo, hivyo sio tatizo kubwa," alisema Jeff Kingston, ambaye anasomea siasa za Japan katika chuo kikuu cha Temple kilichopo mjini Tokyo, katika barua pepe aliloliandikia shirika la habari la  Associated Press.

"Watu wana wasiwasi zaidi juu ya athari za kiuchumi pamoja na kazi zao na idadi ya visa ikizidi kuwa wazi."

Mkurugenzi wa zamani wa masoko wa Kamati ya Kimataifa ya Olimpiki, IOC, Michael Payne, alisema kuwa kucheleweshwa kunaweza kuleta faida kwa IOC na Japan.

"Nini jukwaa bora zaidi kuliko michezo ya Olimpiki wakati ulimwengu umekumbwa na janga la virusi vya Corona," Payne aliliambia shirika la habari la AP katika mahojiano Jumapili iliyopita, kabla ya tangazo la IOC." Una nguvu ambayo itakuwa na nguvu zaidi kwa Japan na wengine wote ulimwenguni. Lakini wakati mgumu wa kufika huko."

Mwenge wa Olimpiki uliwasili siku ya Ijumaa tarehe 20.03.2020 kaskazini mwa Japan. Mbio za mwenge huo zilipangwa kuanza siku ya Alhamisi tarehe 19.03.2020 kutoka eneo hilo lakini ziko katika mashaka. Siku ya Jumapili maelfu ya watu walifurika katika jiji moja la kaskazini mwa Japan kwa ajili ya kushuhudia mwenge huo. Watazamaji walitakiwa kuonyesha vizuizi na kuna taarifa ambazo hazijathibitishwa kuwa mbio za mwenge huo huenda zikacheleweshwa. Waandaaji wa shughuli hiyo ya ukimbizaji mwenge wa Olimpiki siku ya Jumatatu walisema kuwa uamuzi wa ikiwa mbio za mwenge huo zitaendelea unaweza kusubiri.

Jumapili tarehe 22.03.2020 Japan ilikuwa na visa 1,719 vilivyothibitishwa vya virusi hatari vya Corona vikiwemo 712 kutoka katika wasafiri na vifo 43.

Huku Japan ikiwa imefanikiwa kupunguza kasi ya maambukizi ya virusi ya corona, wataalamu wanasema wamepata ongezeko la maeneo ya mjini ambako imekuwa vigumu kufuatilia maambukizi.