1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

MSF yaondoka mpaka wa Beralus na Poland

Hawa Bihoga
7 Januari 2022

Shirika la Madaktari Wasio Mipaka (MSF) limewaondoa wafanyakazi wake katika mpaka wa Poland na Beralus, baada mamlaka nchini Poland kuwazuia kufika maeneo ambayo wahamiaji wanaotaka kuingia mataifa ya Ulaya wamekwama.

https://p.dw.com/p/45Fof
Jahresrückblick BG 2021
Picha: Oksana Manchuk/BelTA/TASS/picture alliance/dpa

Taarifa iliyotolewa na shirika hilo la misaada ya kiutu zinasema kuwa timu ya wafanyakazi wake nchini Lithuania na Belarus wamenyimwa fursa ya kuwafikia wahamiaji na wakimbizi walio mpakani mwa Poland na Beralus licha ya kujaribu kuomba kibali kwa miezi mitatu. 

Taarifa hiyo imeongeza kwamba timu hiyo ilihitaji kuwafikiwa wahitaji waliokwama msituni ambapo wengi kati ya hao wanatafuta hifadhi katika mataifa ya Ulaya.

Mratibu wa dharura wa timu ya wafanyakazi wa MSF nchini Poland, Frauke Ossig, amenukuliwa akisema, tangu mwezi Oktoba shirika lake limekuwa likiomba kufika eneo lililozuiliwa ambapo wahamiaji hao wamekwama huko mpakani lakini kumekuwa hakuna mafanikio yaliopatikana

Grenze Weißrussland Polen | Präsident Alexander Lukaschenko
Rais Alexander Lukashenko wa BelarusPicha: Pavel Bednyakov/dpa/Sputnik/picture alliance

Serikali ya Poland ilijenga vizuizi vya Seng´enge kwenye mpaka wa Belarus na kupiga marufuku watu kufika eneo hilo ikiwemo waandishi wa hababri na hata mashirika ya kutoa misaada ya kiutu, baadhi ya wakimbizi na wahamiaji  ambao walijaribu kuvuka mpaka  na kuingia Poland walikufa.

Ossig ameongeza katika taarifa yake iliyochapishwa katika vyombo vya habari kwamba wanafahamu kuwa bado kuna idadi kubwa ya watu ambao wanajaribu kuvuka mpaka na kujificha msituni na wakihitaji misaada ya kibinadamu, wao wamejitolea kusaidia watu na si kuwahamisha kuwapeleka popote na hawataweza kufanya hivyo.

Mzozo kati ya Belarus na Umoja wa Ulaya 

Irak Erbil | repatriierter Leichnam eines Migranten
Wahamiaji wakiwa mbele ya jeneza la kijana wa Kikurdi aliyekufa mpakani mwa Poland na Belarus.Picha: SAFIN HAMED/AFP/Getty Images

Wengi wanaamini serikali ya Belarus imewaleta wahamiaji hao kutoka  maeneo yalioathirika na  vita hasa kutoka katika nchi za Mashariki ya Kati ikiwemo Iran na Iraq, hii ikiwa ni sehemu ya kulipiza kisasi kwa Umoja wa Ulaya kutokana na vikwazo ilivyowekewa kutokana na kile kinachoitwa ukandamizwaji wa demokrasia katika taifa lake.

Umoja wa Ulaya umekuwa ukiishutumu wazi serikali ya Belarus chini ya Rais Alexander Lukashenko kwa kuwahimiza watu wanaokimbia migogoro na wale wanaosaka maisha bora kutoka mataifa ya Mashariki ya Kati kuitumia nchi yake kama lango kuu kuingia kwenye mataifa ya kanda ya Ulaya kinyume cha sheria.

Maelfu ya wahamiaji na wakimbizi waliokwama wakijaribu kuingia katika Mataifa ya Ulaya wakipitia katika nchi ya Beralus wengi wao wanatajwa kuwa ni jamii ya wakurdi huku idadi kubwa wakiwa ni vijana wanaotafuta maisha bora.