1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mkuu wa WHO aonya kuhusu athari ya mauaji ya kimbari Tigray

20 Oktoba 2022

Mkuu wa Shirika la afya duniani WHO Tedros Adhanom Ghebreyesus ametahadharisha kuwa muda unayoyoma kuzuia kile alichokiita "mauaji ya kimbari" kutokea katika eneo la Tigray Kaskazini mwa Ethiopia.

https://p.dw.com/p/4ISFF
14. Weltgesundheitsgipfel | Tedros Adhanom Ghebreyesus
Picha: Carsten Koall/dpa/picture alliance

Tedros amewaambia wanahabari mjini Geneva kwamba hakuna sehemu yoyote nyingine duniani ambapo watu milioni 6 wamezingirwa kwa takriban miaka miwili.

Tedros ameongeza kuwa huduma za benki, mafuta, chakula, umeme na huduma za afya zinatumika kama silaha za vita.

Tedros, ambaye pia ni waziri wa zamani wa afya na mambo ya nje wa Ethiopia, ameonya kuhusu mgogoro wa afya katika eneo hilo la Tigray na kutoa wito kwa jumuiya ya kimataifa na vyombo vya habari kuzingatia kwa makini mgogoro huo.

Tedros amekuwa akiikosoa serikali ya Ethiopia katika kipindi chote cha mgogoro huo na kukabiliwa na shtuma kwa sababu hiyo. Mapema mwaka huu, serikali ya Ethiopia ilimshtumu kwa kuingilia kati masuala ya ndani ya nchi hiyo na kutozingatia uadilifu na matarajio ya kitaaluma yanayohitajika kutoka ofisi yake.