1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mikhail Gorbachev, Mrusi anaye afariki dunia

31 Agosti 2022

Kiongozi wa mwisho wa uliokuwa Umoja wa Kisovieti Mikhail Gorbachev, Mrusi anayependwa zaidi Ujerumani kwa njia ambayo Urusi haikuwahi kufanya, amefariki akiwa na umri wa miaka 91.

https://p.dw.com/p/4GH7L
	
Michail Gorbatschow gestorben
Picha: CNP/ABACA/picture alliance

Umuhimu wa jukumu lake hauna ubishi, hasa nchini Ujerumani, ambako mshindi huyo wa Tuzo ya Amani ya Nobel anasifiwa kwa kusaidia kuziunganisha tena Ujerumani Mashariki na Magharibi kurudi kuwa taifa moja kubwa na lenye nguvu barani Ulaya.   Gorbachev alipendwa nje ya Urusi kwa njia ambayo hakuwahi kufanyiwa katika nchi yake mwenyewe. Gorbachev alizaliwa mwaka 1931 huko Caucasus Kaskazini, na kupanda cheo kuwa mkuu wa Chama cha Kikomunisti mnamo Machi 1985.

Kiongozi huyo shupavu ambaye wakati huo alikuwa na umri wa miaka 54 alitaka kumaliza udumavu wa Kisovieti, hasa athari yake ya  kiuchumi kuhusiana na Marekani. Katika juhudi za kubadilisha mfumo wa Kisovieti wenye urasimu na ufisadi, alifanya mageuzi chini ya maneno ya Urusi yanayojulikana sana kwa sasa - 'glasnost' kumaanisha uwazi na 'perestroika' kumaanisha marekebisho akiunganisha sera hizi na uhusiano bora na Marekani na washirika wake wa Magharibi. Msimamo wake ulijulikana kama ''Fikra Mpya," na athari yake kwa historia ya ulimwengu haikuweza kuhesabika.

Kusambaratika kwa muungano wa Kisovieti

Muungano wa Kisovieti tayari ulikuwa umeanza kusambaratika wakati Gorbachev alipochaguliwa rais wa kwanza wa urusi mnamo mwaka 1990. Majimbo ya Ulaya Mashariki yalijitenga wakati wa kusambaratika huko mnamo mwaka 1989, huu ukiwa wakati wa kumbukumbu.

Mkataba wa Warsaw, jibu la kijeshi la Muungano huo wa Kisovieti kwa Jumuiya ya kujihami ya NATO, yalikuwa katika hali mbaya na raia wa Ujerumani Mashariki, waliotumiwa na Umoja wa Kisovieti kama taifa la kinga  tangu kumalizika kwa Vita Vya Pili vya Dunia, walikuwa wakitoa wito sio tu wa uhuru na demokrasia, bali kwa Ujerumani iliyoungana tena. Gorbachev alihakikisha kwamba hii ingefanyika kwa amani, licha kwamba wahafidhina wengi wa Kisovieti walionekana kutoridhia . 

Maamuzi binafsi ya Mikhail Gorbachev katika wakati mgumu wa kihistoria hayakupaswi kupuuzwa.

Kansela wa Ujerumani wa wakati huo Helmut Kohl, mfuasi muhimu wa Gorbachev alisema kwamba maamuzi binafsi ya Mikhail Gorbachev katika wakati mgumu wa kihistoria hayapaswi kupuuzwa. Kohl aliongeza kuwa ndani ya saa 24 baada ya kuanguka kwa ukuta wa Berlin, Taasisi inayohusika na usalama ya iliyokuwa Ujerumani Mashariki (Stasi) na idara ya ujasusi ya Urusi (KGB) zilikuwa zikijaribu kumshawishi kwamba wanajeshi wa Kisovieti walikuwa hatarini katika eneo la Ujerumani Mashariki na kwamba jeshi la Kisovieti lilihitajika kuingilia kati, lakini Gorbachev akapinga. Kupanda kwa Gorbachev katika jukwaa la kimataifa kulimsababishia kupoteza ushawishi nyumbani. Mageuzi yake yalifungua njia ya kuporomoka kwa Umoja wa Kisovieti na Wajerumani zaidi, walikuwa wakimsifu kama shujaa kwa mapinduzi ya amani na demokrasia.