1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Messi hakujitokeza kupimwa COVID-19 Barca

Sekione Kitojo
30 Agosti 2020

Lionel Messi  ameshindwa  kufika katika  upimaji wa lazima wa  ugonjwa wa COVID-19 katika viwanja vya Barcelona, vimeandika  vyombo  vya  habari vya Uhispania leo Jumapili(30.08.2020).

https://p.dw.com/p/3hm5S
Champions League | FC Barcelona - FC Bayern München | Lionel Messi
Lionel MessiPicha: picture-alliance/Sven Simon/F. Hörmann

Mchezaji  huyo  maarufu  duniani  mwenye  umri  wa  miaka  33 alikosa  kufika kama ainavyotakiwa , ikiwa  na  maana  kuwa  hataweza  kushiriki  katika mazowezi  ya  kikosi  cha Barcelona  kwa  ajili  ya  msimu  mpya, kwa  mujibu wa  sheria  za  usalama  za  ligi  daraja  la kwanza  nchini  Uhispania , Primera Division.

Spanien F.C. Barcelona | Protest gegen den Abschied von Leo Messi
Mashabiki FC Barcelona wakionesha hali ya kuagana na shujaa wao Lionel Messi baada ya miaka 20 katika klabu hiyoPicha: picture-alliance/NurPhoto/Urbanandsport/J. Valls

Kutoonekana  kwa  Messi  kunachochea uvumi  wa  mzozo  kati  ya  mchezaji  huyo  na klabu. Messi anataka  kuondoka  Barcelona akiwa  mchezaji  huru , akielezea kifungu katika mkataba  wake  ambacho  kinamruhusu  kufanya  hivyo muda  mfupi kabla ya  kumalizika kwa  msimu.

Barca  inapinga  hilo  kwamba  muda  wa  kufanya hivyo umepita Juni 10. Kwa mujibu wa viongozi  wa  Barca , mkataba  wa  Messi , ambao  unakwenda  hadi  Juni 2021 unaeleza kuwa  anapaswa  kueleza  nia  yake  ya  kuondoka  siku  20 kabla ya  kumalizika  msimu.

Spanien F.C. Barcelona | Neuer Coach Ronald Koeman
Kocha mpya wa Barca Ronald KoemanPicha: picture-alliance/AA/A. Puig

Mbali  ya  Messi, wachezaji  ambao wanaoonekana kuhitaji ziada ya  mahitaji  na  kocha wa Barca  Ronald Koeman wamefika kupimwa. Miongoni mwao ni mshambuliaji Luis Suarez, ambaye  anahusishwa na Juventus, Arturo Vidal na  Ivan rakitic, ambae  kuna minong'ono kuwa  anarejea Sevilla.