1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Merkel atetea urathi wake wa Urusi, asema hataomba radhi

8 Juni 2022

Kansela wa zamani wa Ujerumani Angela Merkel ametetea sera yake ya Ukraine na Urusi wakati wa uongozi wake wa miaka 16, akisema hatoomba radhi kwa juhudi zake za kidiplomasia.

https://p.dw.com/p/4CPW7
Deutschland Altkanzlerin Merkel zu Gespräch im Berliner Ensemble
Picha: Fabian Sommer/dpa/picture alliance

Katika matamshi yake ya kwanza muhimu tangu kuondoka madarakani miezi sita iliyopita, Merkel amesema hakuna kisingizio chochote cha kuhalalisha mashambulizi ya kikatili ya Urusi dhidi ya Ukraine, na kwamba hilo lilikuwa kosa kubwa kwa upande wa Urusi.

Merkel ambaye alishughulika na Rais wa Urusi Vladmir Putin katika kipindi chote cha ukansela wake, amepinga madai kwamba yeye na wengine walishiriki ufurahishaji ambao hatimaye uliwezesha uvamizi.

Soma pia: Angela Merkel atajishughulisha na nini baada ya kustaafu?

"Ninachojiuliza, bila shaka ni nini kinaweza kuwa kilikosekana? Je, tungeweza kufanya zaidi kuzuwia janga kama hilo? Nadhani hali hii tayari ni janga, je, ingeweza kuzuwiwa? Na hiyo bila shaka ndiyo sababu naendelea kujiuliza maswali haya," alisema Merkel.

Deutschland Altkanzlerin Merkel zu Gespräch im Berliner Ensemble
Kansela wa zamani wa Ujerumani Angela Merkel, na mwandishi habari Alexander Osanga wakiwa jukwani kabla ya kuanza kwa mahojiano ya kwanza ya Merkel tangu alipoachia ngazi, yaliofanyika ukumbu wa Berliner Ensemble, mjini Berlin, Juni 7, 2022.Picha: DW

Kansela huyo wa zamani ametetea makubaliano ya amani ya mwaka 2015 ambayo yeye na rais wa Ufaransa wa wakati huo Francois Hollande waliongoza mjini Minsk, Belarus, yaliokuwa na lengo la kutuliza mapigano mashariki mwa Ukrainekati ya vikosi vya serikali na waasi wanaotaka kujitenga wanaoungwa mkono na Urusi.

Merkel amekiri kuwa makubaliano hayo hayakutimiza maslahi yote ya Ukraine na kwamba ni watu wachache wanayaunga mkono sasa, huku baadhi wakisema yalijadiliwa vibaya sana, lakini amesisitiza kuwa hakuwa mjinga katika mahusiano yake na Rais Putin.

Soma pia: Marekani yaitaka Urusi kuheshimu makubaliano ya Minsk

"Diplomasia haikuwa mbaya ikiwa haitofanikiwa. Sioni kwamba niseme sasa kuwa haikuwa sahihi, na sitaomba msamaha," alisema Merkel.

Mafanikio ya uongozi wake

Amekumbusha jinsi alivyounga mkono vikwazo vya kiuchumi dhidi ya Urusi baada ya kuinyakua rasi ya Crimea mwaka 2014, pamoja na juhudi za Ujerumani na Ufaransa kuweka hai mchakato wa amani wa Minsk kwa Ukraine.

Merkel amesema vikwazo hivyo vingekuwa na nguvu zaidi, lakini hakukuwa na uungwaji wa wengi kufanya hivyo wakati huo.

Deutschland Altkanzlerin Merkel zu Gespräch im Berliner Ensemble
Kansela wa zamani wa Ujerumani Angela Merkel, na mwandishi habari Alexander Osanga wakiwa jukwani kabla ya kuanza kwa mahojiano ya kwanza ya Merkel tangu alipoachia ngazi, yaliofanyika ukumbu wa Berliner Ensemble, mjini Berlin, Juni 7, 2022.Picha: JOHN MACDOUGALL/AFP

Amesema pia serikali yake ilikuwa na mafanikio kadhaa, na kuongeza kuwa Urusi ilitimuliwa kwenye kundi la mataifa manane tajiri zaidi duniani, G8, na kwamba jumuiya ya kujihami NATO iliweka lengo kwa mataifa wanachama kutenga asilimia 2 ya pato jumla la ndani kwa ajili ya ulinzi.

Soma pia: Mkataba wa Minsk II waanza rasmi

Merkel pia ametetea kwa nguvu uamuzi wa mwaka 2008 wa kutoiweka Ukraine moja kwa moja kwenye njia ya kujiunga na NATO, ambao Rais wa Ukraine Volodymyr Zelenskiy mapema mwezi Aprili aliulaumu kama kosa kubwa ka kimahesabu.

Amesema laiti NATO ingeiruhusu Ukraine kujiunga mara moja mwaka 2008, hatua hiyo ingesababisha uvamizi wa haraka wa Urusi, wakati ambapo Ukraine ilikuwa na uwezo mdogo sana wa kujitetea tofauti na hali ilivyo hivi sasa.

Chanzo: Mashirika