1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
Migogoro

Marekani, washirika waionya Iran kutoishambulia Israel

13 Agosti 2024

Marekani na washirika wake wa Ulaya wameitaka Iran kujizuwia, mnamo wakati hofu ikizidi kuhusiana na shambulio dhidi ya Israel ambalo linaweza kusababisha vita kubwa katika kanda ya Mashariki ya Kati.

https://p.dw.com/p/4jOft
Iran | Kumbukumbu ya kiongozi wa Hamas Ismail Haniyeh
Iran imeapa kuiadhibu Israel kwa mauaji ya Ismail Haniyeh, kiongozi wa kisiasa wa Hamas.Picha: Rouzbeh Fouladi/ZUMAPRESS.com/picture alliance

Wasiwasi unazidi kutanda, huku Marekani ikipeleka nyambizi ya makombora na meli ya kubeba ndege. katika hatua ya kuonyesha uungaji mkono kwa mshirika wake muhimu. Iran na washirika wake wa Lebanon Hezbollah, wameapa kulipa kisasi cha mauaji ya kiongozi wa kisiasa wa Hamas mjini Tehran, na kamanda wa Hezbollah mjini Beirut.

Soma pia: Israel yasema Iran yaandaa mashambulizi ya kulipiza kisasi

Juhudi za kimataifa za kuepusha shambulio la Iran ziliongezeka jana Jumatatu, ambapo Rais wa Marekani Joe Biden, na viongozi wa Ufaransa, Ujerumani, Italia na Uingereza, walitoa tamko la pamoja wakiionya Tehran.

Ismail Haniyeh azikwa nchini Qatar

Ikulu ya White House ilionya kuwa mashambulizi kadhaa makubwa ya Iran na washirika wake yanaweza kutokea wiki hii.

Soma pia: Iran: Tunayo haki ya kuiadhibu Israel kufuatia mauaji ya Haniyeh

Wakati juhudi za kidiplomasia zikiendelea, Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz na Waziri Mkuu wa Uingereza Keir Starmer wamemtaka rais wa Iran Masoud Pezeshkian kutuliza hali. Pezeshkian alisema Jumatatu kuwa nchi yake ina haki ya "kuwajibu wachokozi."

Kiongozi wa Hamas Ismail Haniyeh aliuawa mjini Tehran mwezi uliopita, baada ya kuhudhuria uapisho wa Rais mpya wa Iran, katika shambulio ambalo Iran imeilamu Israel. Israel pia ilimuuwa kamanda wa Hezbollah Fuad Shukr mjini Beirut siku moja kabla, na kuongeza hofu ya kuzuka kwa vita vya kikanda.