1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kashfa za dhulma za kingono zaendelea kujadiliwa Ufaransa

2 Novemba 2021

Maaskofu wa Kanisa Katoliki nchini Ufaransa wameanza kongamano lao la kila mwaka leo Jumane, linalotarajiwa kujadili ripoti iliyoishtua dunia ambayo ilielezea visa vya dhulma za kingono kwa watoto 216,000.

https://p.dw.com/p/42U8H
Frankreich l Tausende von Pädophilen in der französischen katholischen Kirche aktiv
Picha: Julie Sebadelha/ABACAPRESS/picture alliance

Kwa mujibu wa ajenda iliyochapishwa kuhusu kongamano hilo, Maaskofu 120 kutoka kote Ufaransa watatumia mkutano wao wa wiki nzima kujadili juu ya jinsi ya kukabiliana na dhulma na unyanyasaji wa kingono.

Kongamano hilo lililoanza kwa ukimya kama heshima kwa wahanga wa unyanyasaji huo, linafanyika kusini mwa mji wa Lourdes, unaochukuliwa na Kanisa Katoliki kama eneo takatifu.

Kabla ya kongamano hilo, Maaskofu walisema watachunguza uwajibikaji wa Kanisa Katoliki kufuatia ripoti hizo za unyanyasaji pamoja na utaratibu wa kuwalipa fidia wahanga.

Baadhi ya wahanga walialikwa kwenye kongamano hilo, ila wengi walikataa, wakilaani uamuzi wa kujadili kashfa ya dhulma za kingono kuwa moja tu kati ya maudhui watakazozijadili badala ya kuwa maudhui kuu kwenye ajenda yao.