1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Loew aahidi kandanda la kushambulia zaidi

7 Septemba 2020

Mashindano ya UEFA ya Ligi ya Mataifa hayaonekani kuwaendea vyema Ujerumani. Hawajashinda mechi hata moja katika michezo sita lakini Kocha Joachim Loew ana matumaini kuwa hilo litabadilika hivi karibuni.

https://p.dw.com/p/3i7Rh
Fußball | Nations League | Deutschland - Spanien
Picha: picture-alliance/dpa/C. Charisius

Loew ameahidi kuleta kandanda la kushambulia zaidi ambalo litawapa ushindi wao wa kwanza kabisa wa Ligi ya Mataifa, baada ya kutoka sare ya 1 – 1 na Uswisi jana usiku.

Ujerumani ilitoka sare mbili na kupoteza mbili kati ya mechi zao za ufunguzi wa Ligi ya Mataifa miaka miwili iliyopita na wametoka sare mechi mbili  za 1 - 1 msimu huu, dhidi ya Uhispania na kisha Uswisi. Matokeo hayo yanazusha manung'uniko ya kushuka kwa kiwango cha timu ya taifa ya Ujerumani lakini mkurugenzi wa timu Oliver Bierhoff anasema hakuna haja ya kuwa na wasiwasi

Kwanza kabisa, tuna furaha sana kuwa sasa, baada ya muda huu mrefu Zaidi bila kuwa na timu ya taifa, tumejumuika pamoja tena. Na bila shaka tunataka kuleta tena furaha ya timu ya taifa. Hata ingawa tunafahamu watu wana mawazo tofauti na wasiwasi. Lakini tunatumai kuwa wanasubiri kuiona timu yetu ya taifa. Bilas haka tunataka pia kucheza kandanda la kuvutia, la kujituma  na lenye mafanikio.

Fußball: Nations League 2020 I Schweiz - Deutschland Gündogan Tor
Uswisi ilitoka nyuma na kulazimisha sare ya 1 - 1 na UjerumaniPicha: picture-alliance/SvenSimon/V. Witters

Lakini pia kikosi cha Ujerumani kina wachezaji chipukizi ambao ndio sasa wanapata uzoefu wa kushiriki katika mashindano ya kimataifa kitu ambacho Bierhof anasema matunda yake yataonekana katika siku za usoni

Kwetu ni muhimu kutengeza timu mpya ya chipukizi, kuipa nafasi ikue, kumpa mchezaji mmoja au mwingine fursa ya kupata uzoefu zaidi wa mechi za kimataifa. Changamoto ni kuwa makocha hawawezi kuwa na muda wa kufanya kazi na timu. Oktoba na Novemba tuna mechi tatu katika siku nane hadi kumi. Hiyo ni changamoto kubwa. Unaweza tu kufanya mazoezi mara tatu au nne pekee, kama ilivyo sasa tu. Na ujaribu kuwasilisha mawazo na filosofia yako kwa wachezaji katika kipindi kifupi. Lakini tuna furaha sana.

Mechi za Kundi A4 zitaendelea Oktoba 10 wakati Ujerumani itacheza ugenini dhidi ya Ukraine, ambao wako katika nafasi ya pili na pointi tatu baada ya kuwalaza Uswisi nyumbani. Ujerumani watalaalika Uswisi mjini Cologne siku tatu baadaye. Kisha Novemba 14 Ujeurumani itacheza na Ukraine mjini Leipzig na kukamilisha mechi za makundi kwa kupambana na vinara wa sasa Uhispania Novemba 17. Katika mechi hizo, kocha Loew anaweza kuwaweka kikosini nahodha Manuel Neuer, aliyepumzishwa pamoja na wenzake wa Bayern Munich Joshua Kimmich, Leon Goretzka na Serge Gnabry baada ya kushinda Ligi ya Mabingwa Agosti 23.

afp, reuters, dpa