1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kimbunga Helene chaua 210 Marekani

4 Oktoba 2024

Zaidi ya watu 210 wamethibitishwa kufariki dunia kufikia sasa kutokana na kimbunga Helene kilichoyapiga majimbo kadhaa nchini Marekani na kusababisha uharibifu mkubwa.

https://p.dw.com/p/4lP6v
Kimbunga Helene
Athari za Kimbunga Helene katika jimbo la North Carolina, Marekani.Picha: Peter Zay/AA/picture alliance

Maafisa nchini humo wanasema idadi hiyo ya vifo inakipelekea kimbunga hicho kuwa cha pili kwa ukubwa kuwahi kuipiga Marekani katika kipindi cha zaidi ya nusu karne.

Rais Joe Biden kwa siku ya pili mfululizo amefanya ziara katika eneo la kusini mashariki mwa nchi hiyo lililoathirika pakubwa na kimbunga hicho ili kuomboleza na wakaazi wakati ambapo maisha ya mamilioni ya watu yameathirika.

Soma zaidi: Watu 600 hawajulikani walipo North Carolina

Idadi iliyokusanywa na shirika la habari la Ufaransa AFP inaonyesha kuwa watu 212 wamefariki dunia katika majimbo la North na South Carolina, Georgia, Florida, Tennessee na Virginia.

Zaidi ya nusu ya vifo hivyo vimetokea North Carolina, jimbo linalokabiliana na hasara kubwa iliyosababishwa na kimbunga hicho.