1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
JamiiAsia

Marufuku ya matumizi ya bidhaa za plastiki nchini India

1 Julai 2022

India imepiga marufuku matumizi na kutupwa bidhaa za plastiki,kama sehemu ya mpango wa kutokomeza bidhaa hizo kila mahali katika taifa hilo lenye takribani watu bilioni 1.4.

https://p.dw.com/p/4DXnC
Indien | Verbot von Einwegplastikverpackungen
Picha: Satyajit Shaw/DW

Katika hatua ya kwanza,imebainisha vitu 19 vya plastiki ambavyo havina umuhimu sana lakini vinaweza kuwa takataka, hivyo kupekelea kusitisha uzalishaji, uagizwaji, usambazaji na uuzaji. Vitu hivyo ikiwemo vikombe vya plastiki na vijiti vya ice cream. Baadhi ya mifuko ya plastiki itasitishwa na kutakuwepo na mifuko mbadala.

Maelfu ya bidhaa zingine za plastiki  kama chupa za maji, soda na mifuko ya chakula, haijajumuishwa kwenye katazo hilo. Lakini Serikali imeweka malengo kwa wazalishaji kuvichakata tena au kuvitupa baada ya kuvitumia.

Watengenezaji wa plastiki wametoa wito kwa serikali kuchelewesha katazo hilo, kutokana na mfumuko wa bei na upotezaji wa ajira utakaotokea. Lakini waziri wa mazingira nchini India, Bhupender Yadav amesema katika mkutano na waandishi wa habari huko mji mkuu wa India,New Delhi kwamba marufuku hiyo imetangazwa kwa mwaka mmoja.``Sasa muda umekwisha,'' alisema.

 Hii si mara ya kwanza kwa India kupiga marufuku plastiki.Hapo awali marufuku hiyo yalizingatiwa mikoa maalum, na kusababisha kutofautiana katika viwango  vya mafanikio. Marufuku ya nchi nzima inajumuisha sio tu matumizi ya plastiki, lakini pia uzalishaji au uagizaji wake ," alisema Satyarupa Shekhar, mratibu wa kikundi cha Asia-Pacific.

Madhara ya taka za plastiki

Plastiki nyingi hazichakatwi tena duniani na mamilioni ya tani za taka hizo huchafua bahari ya dunia na huathiri wanyamapori.Wanasayansi bado wanajaribu kutathmini hatari zinazosababishwa na vipande vidogo vya plastiki . Mnamo 2020, zaidi ya tani milioni 4.1 za taka za plastiki zimezalishwa nchini India, kulingana na shirika  la kudhibiti uchafuzi wa mazingira la serikali.  

Usimamizi mbaya wa taka zinazoendelea kushamiri kwenye miji na vijiji inaonyesha namna ambavyo taka nyingi hazijachakatwa na kupelekea kuchafua mazingira.Takribani tani milioni 13 za taka za plastiki hazikuchakatwa na zilitapakaa kwenye taifa la hilo la Asia Kusini mnamo 2019, ikiwa imeongoza duniani.

Utengenezaji wa plastiki hutoa gesi chafu zinazo ongeza joto duniani ndani, na India ni nchi yenye viwanda vinavyotengeneza zaidi ya tani 243,000 za taka za plastiki kila mwaka. Hivyo kupunguza utengenezaji wa taka za plastiki katika shughuli za kiuchumi kwa asilimia 45 ni muhimu nchini  India ili kufikia lengo  katika miaka minane.

Utafiti hivi karibuni,umeonyesha kuwa zaidi ya viungio vya kemikali 8,000 vinatumika kwenye usindikaji wa plastiki, na hutoa gesi chafu. Plastiki nyingi haziwezi kuchakatwa tena, mara nyingi huteketezwa na hutumika kama mafuta katika mitambo ya nishati.

Indien | Verbot von Einwegplastikverpackungen
Picha: Satyajit Shaw/DW

Ravi Agarwal, mkurugenzi wa kikundi cha Toxics Link, yenye makao yake New Delhi, kiliongeza kuwa marufuku hiyo ilikuwa na  ``mwanzo mzuri,'' lakini mafanikio yake yatategemea namna itakavyotekelezwa. Utekelezaji wa sheria utadhibitiwa na majimbo na manispaa ya miji.India ilisema kuwa bidhaa za plastiki zimepigwa marufuku huku ikizingatia upatikanaji wa njia mbadala ikiwemo vijiko vya mbao,

Moti Rahman,  mwenye umri wa miaka 40, ni mfanyabiashara mdogo wa mbogamboga huko New Delhi, amesema kwamba anakubaliana na marufuku hiyo, lakini kama mifuko ya plastiki itasitishwa bila kuwa na upatikanaji rahisi na gharama nafuu kwa mifuko mbadala, biashara yake itaathiriwa. Aliongezea kuwa,``plastiki inatumika katika kila kitu."