1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUgiriki

Waliofariki dunia katika ajali ya treni Ugiriki wafikia 42

2 Machi 2023

Mkuu wa kituo cha treni aliyekuwa zamu wakati wa ajali mbaya zaidi ya treni nchini Ugiriki leo (2.023.2023) atafika mbele ya hakimu wa eneo la kati mwa jiji la Larissa kutoa ushahidi wake kuhusu ajali hiyo

https://p.dw.com/p/4OA7P
Griechenland Zugunglück Tempe
Picha: George Kidonas/InTime News/AP/picture alliance

Mwanaume huyo mwenye umri wa miaka 59, atafika mbele ya hakimu kuelezea jinsi treni iliyokuwa na zaidi ya abiria 350 ilivyoruhusiwa kuendeshwa katika njia moja na treni ya kusafirisha mizigo kwa kilomita kadhaa. Haya yanajiri wakati maafisa wa serikali wakichunguza hali zilizosababisha ajali hiyo ya treni iliyokuwa ikielekea katika mji wa Kaskazini wa Thessaloniki ilipogongana na treni ya kusafirisha mizigo iliyokuwa inakuja kutoka upande tofauti lakini katika njia moja ya treni.

Juhudi za uokoaji zaelendelezwa 

Maafisa wa uokoaji leo waliendeleza juhudi za kuwatafuta manusura huku wakisema kwamba hawajawahi kushughulikia janga kubwa kama hili. Miili mingi iliteketea kabisa na baadhi ilitambuliwa kwa kuunganisha vipande.  Hapo jana jioni, maandamano yalifanywa katika kituo cha treni cha Thessalonik, katika mji wa Larissa na nje ya ofisi za kampuni ya reli inayomilikiwa na Italia ya Hellenic mjini Athens  ambapo waandamanaji walirusha mawe katika jengo hilo na polisi.

Mjini Larissa, waandamanaji walifanya mkesha wa maombolezo na kuleta maua meupe kuunda jina Tempe, jina la bonde ambalo ajali hiyo ilitokea. Waziri mkuu wa nchi hiyo Kyriakos Mitsotakis amesema ajali hiyo ilikuwa mbaya na haijawahi kuwa na mfano wake nchini Ugiriki huku akiahidi kwamba uchunguzi kamilifu utafanywa.

UK Besuch des griechischen Premierminister Kyriakos Mitsotakis in London
Waziri mkuu wa Ugiriki Kyriakos MitsotakisPicha: Justin Ng/Avalon/Photoshot/picture alliance

Mitsotakis asema ajali ilisababishwa na makosa ya kibinadamu

Katika hotuba kupitia televisheni hapo jana jioni baada ya kuzuru eneo la mkasa, Mitsotakis alisema dalili zote zinaonesha kuwa kisa hicho kilitokana na makosa ya kibinadamu. Serikali imetangaza siku tatu za maombolezo ya kitaifa.

Huku hayo yakijiri, waziri wa uchukuzi Kostas Karamanlis amejiuzulu masaa machache baada ya ajali hiyo. Katika taarifa kwa umma, Karamanlis amesema kuwa wakati kitu kibaya kama hicho kinapotokea, hawawezi kuendelea kana kwamba hakuna kilichotokea.

Mapungufu ya viwango vya usalama katika njia hiyo ya treni  yamejulikana kwa miaka mingi sasa.

Lakini wanachama wa vyama vya wafanyakazi wamesema mapungufu ya viwango vya usalama katika njia ya treni ya kutoka Athens kuelekea Thessaloniki yamejulikana kwa miaka mingi sasa. Katika barua wazi mwezi uliopita, wafanyakazi wa sekta hiyo ya uchukuzi wa treni, walisema mifumo ya ufuatiliaji wa usalama bado haijakamilishwa na ina usimamizi mbaya. Msimamizi wa usalama alijiuzulu mwaka uliopita na kusema uimarishaji wa miundo mbinu haujakamilika tangu mwaka 2016 na kwamba kasi ya treni ya hadi kilomita 200 kwa saa sio salama.