1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Usindi kwa Kikosi cha pili cha Bayern Munich

16 Oktoba 2020

Bayern Munich imeilaza FC Düren 3-0 FC ugani Alianz Arena, katika mechi za kombe la Ujerumani. Mkufunzi Hansi Flick alilazimika kutumia kikosi cha pili kupumzisha kikosi cha kwanza

https://p.dw.com/p/3k1lw
DFB Pokal | FC Düren gegen Bayern München
Picha: Christof Stache/AFP

Kikosi cha pili cha Bayern Munich kimeipa kichapo cha mabao 3-0 FC Düren usiku wa Alhamisi ndani ya uga wa Alianz Arena, katika mechi za kombe la Ujerumani, - DFB Pokal. Kocha Hansi Flick alilazimika kutumia kikosi cha pili ili kupumzisha kikosi cha kwanza kwa minajili ya ratiba ya ligi kuu ya ujerumani Bundesliga.

Mshambuliaji mpya Eric Maxim Choupo-Moting, aliyesajiliwa bila malipo kutoka Paris Saint-Germain, alidhihirisha umahiri wake kwa kupachika wavuni mabao mawili kwenye mechi yake ya kwanza, pia akashinda penalti katika ushindi wa 3-0.

Wachezaji wapya waliojiunga na Bayern Munich Alexander Nübel, Bouna Sarr, na Marc Roca walipata nafasi ya kucheza mechi yao ya kwanza.

Choupo-Moting alionekana kiungo kamili, iwapo Robert Lewandowski atahitaji kupumua au, hata akiwa na jeraha. Kimo chake kilitoa nafasi nzuri kwake kupanga pasi nzuri, akionesha harakati nzuri za kutafuta kufunga mabao.

DFB Pokal - FC Duren vs. Bayern Munich
Picha: Andreas Gebert/Reuters

Mabao ya Choupo-Moting yalitikisa wavu kunako dakika ya 24 na 75 mtawalia.

"Ilikuwa mechi nzuri ya kwanza, ninafuraha kwa kufunga mabao yangu mawili," mchezaji huyo wa kimataifa wa Cameroon alisema baada ya mechi.

Bouna Sarr atakuwa pia amempa faraja nyingi Flick, akimtengenezea Choupo-Moting nafasi nzuri ya kufunga mabao, vile vile kipa mpya Nübel alijitahidi kuweka rekodi ya kutofungwa katika mechi hiyo.

Safu ya ulinzi Jerome Boateng, Niklas Süle walimakinika pamoja na mzoefu Thomas Müller ambaye alifunga bao lake la pili la msimu huu dakika ya 36.

Douglas Costa, amerudi Bayern kutoka Juventus nchini Italia na pia Flick inaoneka alirishishwa na mchezo wake.

"Kwa sasa tumeridhika, lazima tuone kwamba wanafika kiwango cha asilimia 100 hatua kwa hatua," alisema.

Bayern sasa wanaingia katika kipindi kigumu katika ratiba yao ya michuano itacheza mechi saba ndani ya kipindi cha siku 22. Jumamosi hii watashuka dimbani kuivaa Arminia Bielefeld katika mechi za Bundesliga.