1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaJamhuri ya Kongo

Upinzani Kongo kuafikiana kusimamisha mgombea mmoja?

Amina Mjahid
22 Novemba 2023

Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo Felix Tshisekedi anagombea awamu nyingine ya urais katika uchaguzi wa mwezi Desemba akipambana na wagombea wengine 20 kutoka vyama vya upinzani, lakini usalama ni changamoto kubwa

https://p.dw.com/p/4ZIG8
Demorkasia | Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo Felix Tshisekedi
Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo Felix TshisekediPicha: Isa Terli /AA/picture alliance

Kampeni ya kuelekea uchaguzi wa Disemba 2023, nchini Congo zilizinduliwa nchini humo siku ya Jumapili ya tarehe 19 Novemba. Lakini kampeni hizi zinaendelea kukiwa na migogoro katika mikoa tofauti katika taifa hilo la Afrika.

Rais Felix Tshisekedi, aliye na miaka 60 na aliyeingia madarakani mwaka 2018, kufuatia uchaguzi uliokuwa na utata anagombea tena kutetea kiti chake na muhula mwengine wa pili.

Siku hiyo ya Jumapili alizindua rasmi kampeni yake katika uwanja wa Martyr mjini Kinshasa, iliyohudhuriwa na zaidi ya wafuasi wake 80,000 licha ya mvua kubwa iliyokuwa ikinyesha.

Tshisekedi alisifia mafanikio ya serikali yake akisisitiza kwamba sera yake ya elimu ya bure imefanikiwa pakubwa, licha ya upinzani kutoka kwa  chama cha FCC kusema kwamba sitofanikiwa.

Rais huyo anaetetea kiti chake aliwaomba wafuasi wake wampe nafasi nyengine ili aweze kuendeleza mafanikio yake.

Mpango wa kugawana madaraka aliyokuwa nao na mtangulizi wake Joseph Kabila wa chama cha FCC ulimruhusu Tshisekedi kuapishwa kama rais mwaka 2019.

Soma pia:Kongo: Kipenga cha kampeni za uchaguzi chapulizwa

Rais huyo amelalamika kuwa mpango huo ulitatiza utendaji wa serikali yake kwa miaka miwili ya uongozi wake kabla ya kuvunjika mwaka 2020.

Kwa uchaguzi wa mwaka 2023 rais huyoameunda muungamo mpya unaoitwa Sacred Union of the Nation. Esther Mampuya ni mwanaharakati wa muungano huo mpya wa Tshisekedi aliyeshiriki uzinduzi wa kampeni zake mjini Kinshasa, mesema kile wanachokitaka ni rais wao kupewa nafasi ya kuongoza muhula wa pili kuonesha kile anachoweza kuifanyia nchi yake na kwamba anaweza kufanya mabadiliko ambayo watu wanadhani ni magumu kufanya.

Upinzani kusimamisha mgombea mmoja Kongo?

Jumla ya watu 26 wanagombea urais akiwemo Martin Fayulu aliye na miaka 66 aliyewahi kuwa mkuu wa kampuni ya mafuta ya Exxon Mobil.

Fayulu, aliyemaliza wa pili katika uchaguzi wa rais mwaka 2018 hakuyakubali matokeo hayo wakati huo na kudai kuibiwa ushindi. Siku hiyo ya Jumapili hata yeye alizindua kampeni yake katika eneo la Bandundu Kaskazini Mashariki mwa Kinshasa.

Kando na hilo moja ya hasimu mkuu wa rais Tshisekedi ni Moise Katumbi aliyezindua kampeni yake katika mji wa Kisangani mkoani Tshopo.

Demokrasia | Wagombea urais Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo- 2023
Wagombea urais Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo- 2023Picha: AFP/Getty Images, picture alliance, G. Kusema, DW

Katumbi, mfanyabiashara tajiri na gavana wa zamani wa mji huo tajiri kwa madini ya shaba anaungwa mkono na Waziri Mkuu wa zamani Augustin Matata Ponyo, aliyejiondoa katika kinyan'ganyiro hicho.

Wawakilishi kutoka kwa vyama vikuu vya upinzani walianzisha mazungumzo nchini Afrika Kusini wiki iliyopita ya kushiniiza upatikanaji wa mgombea wa pamoja kushindana na Tshisekedi. Tayari Matata Ponyo ameituhumu serikali ya Kongo kwa kuwa na njama ya kuiba kura.

Soma pia:Upinzani Kongo waazimia kuungana kuelekea uchaguzi Desemba

Huku hayo yakiarifiwa mapigano ya mara kwa mara yamekuwa yakishuhudiwa Mashariki mwa taifa hilo kwa zaidi ya miongo mitatu sasa, mzozo uli-- anza tena hivi karibuni baada ya kundi la waasi wa M23 linalodaiwa kuungwa mkono na Rwanda lilipodhibiti maeneo mengi ya Kivu Kaskazini.

Kuna wasiwasi kwamba kampeni za uchaguzi huenda zikatatizwa na machafuko katika sehemu tofauti nchini humo. Rwanda imeendelea kukanusha kwamba haiwafadhili wala kuwaunga mkono waasi wa M23.

Watu milioni 44 kati ya milioni 100 ya Idadi Jumla ya watu nchini humo wamesajiliwa kushiriki uchaguzi huo uliopangiwa kufanyika tarehe 20 Desemba.

Katika uchaguzi huo, wapiga kura pia watawachagua wabunge, madiwani na viongozi wa serikali za mitaa katika nchi hiyo iliyo na rasilimali kubwa lakini inayokumbwa na migogoro ya mara kwa mara pamoja na ufisadi.

Vyama vya siasa vya upinzani Afrika vimetekeleza wajibu wao?