1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Scholz atembelea Solingen kulikofanyika shambulio la kisu

26 Agosti 2024

Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz ameutembelea mji wa Solingen baada ya mwanamume mmoja raia wa Syria anayeshukiwa kuwa na uhusiano na kundi linalojiita Dola la Kiislamu (IS) kuwashambulia watu kwa kisu.

https://p.dw.com/p/4jvDx
Ujerumani Solingen | Olaf Scholz awakumbuka waliouawa kwa kisu
Katikati: Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz katika mji wa Solingen kuwakumbuka waliouawa kwa kushambuliwa kwa kisuPicha: Thomas Banneyer/dpa/picture alliance

Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz ametoa heshima kwa wahanga wa shambulio la kisu katika jiji la Solingen. Maua, mishumaa na ujumbe wa maandishi vimetanda barabarani tangu siku ya Ijumaa usiku.

Solingen ni jiji lenye takriban watu 160,000, liko kati ya miji ya Duesseldorf na Cologne.

Ujerumani Solingen | Olaf Scholz awakumbuka wahanga wa mashambulizi ya kisu
Maua na mishumaa katika eneo yalikofanyika mashambulizi ya kisuPicha: Jana Rodenbusch/REUTERS

Mshukiwa ambaye ni raia wa Syria mwenye umri wa miaka 26 amewekwa kizuizini tangu Jumapili jioni anakabiliwa na tuhuma mbalimbali, ikiwa ni pamoja na kuwa mwanachama wa kundi la kigaidi IS, na mauaji.

Soma Pia: Polisi ya Ujerumani yapata kifaa inachoshuku kimetumika katika shambulio la Solingen 

Waendesha mashtaka wa Ujerumani wanaopambana na ugaidi wanamchunguza mtu huyo anayeitwa Issa al H.

Kundi la kigaidi la IS lilisema katika taarifa yake siku ya Jumamosi kwamba mmoja wa wanachama wake amefanya shambulio hilo ili "kulipiza kisasi" kwa niaba ya waislamu wa Palestina na wa kila mahali.

Mashambulio hayo yalifanyika siku ya ijumaa jioni, wakati wa tamasha katika jiji  Solingen ililopo magharibi mwa Ujerumani. Watu watatu waliuawa, wengine wanane walijeruhiwa na wanne kati yao wakiwa katika hali mahututi.

Ujerumani Solingen | Olaf Scholz katika mji yalikotokea mashambulizi ya kisu
Katikati: Kansela wa Ujerumani Olaf ScholzPicha: Henning Kaiser/REUTERS

Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz ameyaelezea mashambulio hayo ya kisu kama uhalifu mbaya na amesema ni lazima nguvu kamili za sheria zitumike.

Kutokana na shambulio hilo baya la kisu katika mji wa Solingen, upande wa upinzani umeongeza shinikizo la kupinga wahamiaji, Friedrich Merz, kiongozi wa chama cha mrengo wa kulia cha Christian Democratic Union (CDU), ametoa wito wa kufanyika uchaguzi ili kusitisha mara moja upokeaji wa wakimbizi kutoka Syria na Afghanistan.

Waziri wa mambo ya ndani wa jimbo la North Rhine Westphalia, Herbert Reul, liliko jiji la Solingen ametaka ukaguzi uimarishwe katika mipaka ya Ujerumani yote na hatua zichukuliwe za kuwakataa wakimbizi.

Soma Pia: Waziri wa ulinzi wa Ujerumani alaani shambulio la kisu Solingen

Mwanasiasa huyo wa kihafidhina amesisitizta kuwa ni muhimu sana kuchukua hatua za kupunguza wahamiaji. Amesema ni sahihi kuondolewa nchini Ujerumani wakimbizi ambao maombi yao hayajakubaliwa na hasa wa kutoka Afghanistan na Syria anakotoka mshukiwa wa mashambulio ya Solingen.

Kiongozi wa chama cha CDU Friedrich Merz
Friedrich Merz, kiongozi wa chama cha mrengo wa kulia cha Christian Democratic Union (CDU)Picha: Michael Kappeler/dpa/picture alliance

Katibu mkuu wa chama kinachotawala cha Ujerumani Social Democrats (SPD), Kevin Kühnert, amepinga wito wa upinzani.

Kikao maalum cha bunge kitafanyika katika Bunge la jimbo la NorthRhine Westphalia baadaye wiki hii kufuatia mashambulizi ya kisu katika mji wa Solingen, vyama vya (SPD) na (FDP) vimesema leo Jumatatu.

Vyanzo: DPA/AFP