1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaAsia

Mkuu wa majeshi wa Cambodia arithi uwaziri mkuu

7 Agosti 2023

Mfalme wa Cambodia amemuidhinisha Mkuu wa Majeshi, Hun Manet, kuwa waziri mkuu kufuatia kujiuzulu hivi karibuni kwa baba yake, Hun Sen, baada ya kuitawala nchi hiyo kwa mkono wa chuma kwa takribani miaka 40.

https://p.dw.com/p/4Uqhb
Kambodscha | Hun Manet
Picha: Heng Sinith/AP Photo/picture alliance

Tangazo hilo limetolewa kupitia amri iliyotiwa saini na Mfalme Norodom Sihamoni na kusambazwa kwa vyombo vya habari.  

Idhini hiyo ya Mfalme inaamaanisha Hun Manet ndiye atakuwa kiongozi mpya wa Cambodia na atachukua rasmi nafasi ya waziri mkuu hapo Agosti 22 wakati bunge litakapokutana kwa mara ya kwanza. 

Soma zaidi: Waziri Mkuu Cambodia kumrithisha madaraka mwanaye?
Kiongozi wa upinzani Cambodia afungwa miaka 27 jela kwa uhaini

Katika ujumbe wa shukrani alioutoa kupitia mtandao wa Telegram, kiongozi huyo mteule ameahidi kuleta mageuzi nchini Cambodia na kuendelea kuboresha maisha ya watu. 

Atachukua wadhifa huo baada ya baba yake, Hun Sen, kutangaza ghafla kuwa atawachia nafasi ya waziri mkuu kiasi mwezi mmoja tangu chama chao cha CPP kupata ushindi mkubwa katika uchaguzi wa Julai ambao, hata hivyo, ulikosolewa na jumuiya ya kimataifa.