1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

HRW yaitaka Kongo kupanua uchunguzi wa mauaji mjini Goma

30 Agosti 2024

Mamlaka nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo zinapaswa kupanua uchunguzi wao dhidi ya maafisa wa usalama waliohusika na mauaji ya watu wengi mashariki mwa nchi hiyo mwaka mmoja uliopita.

https://p.dw.com/p/4k5pW
Maafisa wa jeshi la Kongo washika doria mjini Goma, jimboni Kivu Kaskazini, eneo linalokabiliwa na vurugu la makundi ya waasi mnamo Aprili 11,2024
Maafisa wa jeshi la Kongo washika doria mjini GomaPicha: Wang Guansen/Xinhua/picture alliance

Lewis Mudge, mkurugenzi wa Human Rights Watch katika eneo la Afrika ya Kati, amesema mwaka mmoja baadaye, mamlaka nchini Kongo imefanikiwa kuwashtaki watu kadhaa kwa mauaji ya Goma ya mwaka 2023, lakini hakujafanywa uchunguzi wa kutosha na hakuna fidia iliyolipwa kwa waathiriwa.

Mudge apendekeza hatua za kuzuia unyanyasaji wa baadaye

Mudge ameongeza kuwa kuanzisha taasisi huru ya kuchunguza mienendo ya polisi na kuwaadhibu ipasavyo wale wote waliohusika ni muhimu ili kuzuia unyanyasaji kama huo katika siku zijazo.

Soma pia:Watu 10 wauawa katika shambulio la ADF mashariki mwa Kongo

Mfuasi wa vuguvugu moja ambaye mkewe aliuawa amesema angependa kulipwa fidia kwa hasara waliyopata na kuongeza kuwa kulea watoto saba bila mama yao ni jambo gumu sana kwake. Mfuasi huyo pia amesema wanahitaji msaada.

Kongo inapaswa kushughulikia mikakati ya kudhibiti makundi ya watu

Human Rights Watch imesema, mbali na kupanua uchunguzi dhidi ya wale waliohusika na mauaji yaliofanywa na maafisa wa serikali na kutoa fidia kwa waathiriwa, mamlaka ya Kongo inapaswa kushughulikia mikakati yake ya kudhibiti makundi ya watu.

Watu waliopoteza makazi yao mjini Munigi, viungani mwa Goma wanasubiri msaada wa chakula wa shirika la UNICEF mnamo Desemba 5, 2022
Watu waliopoteza makazi yao mjini Munigi, viungani mwa GomaPicha: Guerchom Ndebo/AFP

Shirika hilo limeongeza kuwa kwa ujumla,  jeshi halipaswi kutumika kwa ajili ya utekelezaji wa sheria, kazi ambayo polisi wamepata mafunzo bora na kuongeza kuwa vikosi vyovyote vya usalama vinavyotumiwa kudhibiti umati vinapaswa kupokea mafunzo bora, vifaa na usimamizi unaofaa.

Soma pia:Usitishaji mapigano mashariki mwa Kongo waafikiwa

Human Rights Watch pia imesema serikali ya Kongo inapaswa kutafuta msaada wa kimataifa ili kuhakikisha kwamba vikosi vyake vya usalama vinazingatia viwango vya kikanda na kimataifa kuhusu matumizi ya nguvu.

Mudge amesema waathiriwa wa mauaji ya Goma wanasubiri uwajibikaji na wale wote waliohusika bila ya kujali vyeo vyao wanapaswa kushitakiwa na waliojeruhiwa kufidiwa.

Vikosi vya usalama vya Kongo viliwauwa takriban watu 57

Mnamo Agosti 30, 2023, vikosi vya usalama vya Kongo viliwauwa takriban watu 57 huko Goma, mji mkuu wa jimbo la Kivu Kaskazini.

Wengi wao walikuwa washiriki wa kundi la kidini la , the Natural Judaic and Messianic Faith Towards the Nations (Foi Naturelle Judaique et Messianique vers les Nations) waliokuwa wakipanga maandamano dhidi ya ujumbe wa kulinda amani wa Umoja wa Mataifa nchini humo MONUSCO.Soma pia:Mapigano yaanza tena mashariki mwa Kongo kati ya jeshi na M23

Jopo la wataalamu wa Umoja wa Mataifa na Human Rights Watch waligundua kwamba idadi halisi ya waliofariki ina uwezekano wa kuwa kubwa zaidi. Mnamo mwezi Oktoba, mahakama ya kijeshi iliwapata na hatia ya mauajiwanajeshiwanne, akiwemo kamanda mmoja mkuu, lakini hakuna uchunguzi zaidi unaoonekana kuendelea na hakuna waathiriwa waliopata fidia.