1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Binadamu apandikizwa figo ya nguruwe kwa mara ya kwanza

22 Machi 2024

Madaktari nchini Marekani wametangaza kwamba mwanaume mmoja wa miaka 62 aliyekuwa mgonjwa wa figo amekuwa binadamu wa kwanza kupokea figo mpya aliyopandikizwa kutoka kwa nguruwe aliyebadilishwa vinasaba

https://p.dw.com/p/4e2Gp
Upandikizaji wa figo
Madaktari nchini Marekani wamefaanikisha kwa mara ya kwanza kupandikiza figo ya nguruwe kwa binadamu kwa mara ya kwanzaPicha: Massachusetts General Hospital/AP/picture alliance


Madaktari nchini Marekani wafanikisha kwa mara ya kwanza upandikizaji wa figo ya nguruwe kwa binadamu.

Madaktari katika hospitali kuu ya Boston huko Massachusetts nchini Marekani wametangaza kwamba mwanaume mmoja wa miaka 62 aliyekuwa mgonjwa wa figo katika hatua ya mwisho amekuwa binadamu wa kwanza kupokea figo mpya aliyopandikizwa kutoka  kwa nguruwe aliyebadilishwa vinasaba.

Soma zaidi: Steinmeier kumpa mkewe figo

Taarifa ya hospitali hiyo imesema kwamba upasuaji huo uliochukua takribani saa nane uliofanywa Machi 16, umeweka alama kubwa na hatua muhimu katika jitihada za kutoa viungo vinavyopatikana kwa urahisi zaidi
kwa wagonjwa.

Kwa sasa mgonjwa aliyepandikizwa figo hiyo ya Nguruwe, Richard Slayman ambae ni mkazi wa Weymouth, huko Massachusetts, yuko katika hali nzuri na anatarajiwa kuruhusiwa hospitalini hivi karibuni.

USA Boston 2024 | Weltweit erste Transplantation einer genetisch modifizierten Schweineniere in einen lebenden Menschen
Kwa mara ya kwanza binadamu ameweza kupandikizwa figo ya nguruwe na madaktari wanasema kwa sasa mgonjwa huyo wa figo anaendelea vizuri na ataruhisiwa hivi karibuniPicha: AP Photo/picture alliance

 Dkt. Jim Kim, mkurugenzi wa upandikizaji wa figo na kongosho hukoLos Angeles amesema kuwa wataalam sasa wanafikiria kuendelea zaidi na uvumbuzi wa matokeo ya muda mrefu ya upandikizaji wa figo kutoka kwa mnyama hadi kwa binadamu.

Huu ni upandikizaji wa pili kufanyika

Hii ni mara ya pili kwa Slayman kufanyiwa upandikizaji wa figo, mwaka  2018 alifanyiwa upandikizaji wa figo ya binadamu lakini baada ya miaka mitano kiungo hicho muhimu kilishindwa kufanya kazi.

Figo hiyo aliyowekewa ilitolewa kwenye maabara huko Cambridge, Massachusetts, kutoka kwa nguruwe ambaye alikuwa amebadilishwa vinasaba na kuondolewa kwa jeni zenye madhara kwa mpokeaji.

Tazama  zaidi: 

Afya: Upandikizaji wa figo kwa njia ya kisasa

Figo kama hizo zilizobadilishwa vinasaba zimetajwa kuwa zinafanya kazi pia kwa wanyama wengine pia kwa mafanikio, Kwa mujibu wa jarida la nature  watafiti wanaeleza kwamba nyani mmoja aliyepandikizwa figo kama hiyo anakadiriwa kuishi kwa wastani wa walau siku 176 na wakati mwingine hata zaidi ya miaka mwili.
Madaktari wamesema kuwa upasuaji huo unaashiria maendeleo katika upandikizaji wa viungo kutoka wanyama kwenda kwa binadamu na hii inaonyesha kuwa hatua hiyo inatoa mwanga wa kupata msaada kwa maelfu ya watu wenye changamoto hiyo.

Kulingana na taasisi ya Marekani yenye mtandao inayoshughulikia viungo ni kwamba  zaidi ya Watu 100,000 nchini Marekani wanasubiri kupandikizwa viungo huku figo ikiwa ni hitaji kubwa zaidi.

Timu ya Chuo Kikuu cha Maryland mnamo Januari 2022 ilipandikiza moyo wa nguruwe kwa bibi wa miaka 57 aliyekuwa na ugonjwa wa moyo lakini alikufa baada ya miezi miwili tu baada ya kupandikizwa moyo huo.