1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Marekani yatangaza vikwazo dhidi ya 'mtandao wa al-Shabaab'

Bruce Amani
11 Machi 2024

Wizara ya fedha ya Marekani imetangaza vikwazo dhidi ya kile ilichosema ni mtandao wa kimataifa wa uchangishaji na utakatishaji fedha kwa ajili ya kundi la al-Shabaab linaloendesha harakati zake nchini Somalia.

https://p.dw.com/p/4dP01
Wapiganaji wa al-Shabaab
Katika picha hii ya tarehe 17 Februari 2011, wapiganaji wa al-Shabaab wanaonekana wakiwa na silaha zao.Picha: picture alliance / AP Photo

Vikwazo hivyo vilivyotangazwa siku ya Jumatatu (Machi 11), viliyalenga makundi 16 na watu binafsi kote katika eneo la pembe ya Afrika, Umoja wa Falme za Kiarabu na Cyprus.

Soma zaidi: Somalia yavunja masharti ya vikwazo vya silaha

Taarifa ya wizara hiyo ilisema hatua hiyo, inayofuatia vikwazo vya Marekani vya Oktoba 2022 dhidi ya mtandao tofauti wenye mafungamano na al-Shabaab, inazifungia mali zozote wanazomiliki nchini Marekani na kuwazuia Wamarekani kufanya biashiara nao.

Soma zaidi: Jeshi la AMISOM laongezewa muda Somalia

Wizara ya fedha ya Marekani ilisema al-Shabaab, ambayo Washington inaichukulia kuwa kundi la kigaidi, hutengeneza zaidi ya dola milioni 100 kwa mwaka, ikiwemo kuwatoza hela wafanyabiashara wa ndani.