1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Jeshi la DR Kongo lawazuiwa waasi wa M23 kuutwaa mji wa Sake

8 Februari 2024

Jeshi la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo jana lilizima jaribio la waasi wa M23 waliokuwa tayari wameukaribia mji wa Sake kilomita 27 kutoka Goma mashariki mwa taifa hilo la kati mashariki ya Afrika.

https://p.dw.com/p/4c9z6
Kongo | Uganda
Wanajeshi wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na Uganda kwenye operesheni ya pamoja mashariki mwa Kongo.Picha: Alain Uaykani/Xinhua/picture alliance

Vyanzo vya ndani vimeeleza kuwa watu wasiopungua saba wamefariki katika mji huo baada ya bomu kuangukia eneo la makaazi.

Raia waliobaki katika mji huo wamesema kuwa hali ni tulivu tangu asubuhi ya leo.

Gavana wa kijeshi kupitia msemaji wake wa kiraia Jymi Nziali aliyezuru mji wa Sake jana jioni ameviambia vyombo vya habari kuwa hali ni tulivu kwa sasa na kuwa wananchi wameanza kurejea majumbani.

Soma zaidi: Wanne wauawa, 25 wajeruhiwa kwa mabomu ya M23

Hata hivyo, ripoti zimesema mapigano mengine makali yanaendelea hadi mchana huu kwenye mji wa Kibumba wilayani Nyiragongo karibu kilometa 22 kaskazini mashariki mwa mji wa Goma ambako wapiganaji vijana wazalendo wanaoungwa mkono na jeshi la kongo wanakabiliana na M23. 

Raia wa eneo hilo wameeleza kusikia milio ya makombora tangu asubuhi wakati vijana wazalendo walikuwa wakizilenga ngome za M23 kwenye vijiji vya Rwibiranga na Ruhunda mbali kidogo na Kibumba ya kati.

Waasi wa kundi M23 walirudi katika eneo hilo mwaka moja baada ya kuondoka  kwa kikosi kutoka nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki kama ilivyotakiwa na utawala wa Kinshasa.