1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaIsrael

Guterres aitaka Israel kuondoa vizingiti vinavyozuia misaada

Lilian Mtono
24 Machi 2024

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amesema leo kwamba Israel haina budi kuondoa vizingiti vilivyosalia pamoja na vituo vya ukaguzi ili kufanikisha ufikishwaji wa misaada Gaza.

https://p.dw.com/p/4e4WY
Antonio Guterres akiwa kwenye mkutano wa masuala ya nyuklia, mjini Brussels Machi 21, 2024
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ameiomba kwa mara nyingine Israel kuangazia namna ya kuondoa vizingiti ili kuruhusu uingizwaji wa misaada huko GazaPicha: Omar Havana/AP/picture alliance

Guterres ametaka Israel kuweka mazingira rahisi ili kuhakikisha misaada muhimu inaingizwa kwenye Ukanda wa Gaza unaokabiliwa na kitisho cha njaa.

Guterres amesema hayo katika mkutano na waandishi wa habari mjini Cairo sambamba na Waziri wa Mambo ya Nje wa Misri, Sameh Shoukry na kutoa wito kwa mara nyingine wa usitishwaji wa mapigano ili kupunguza madhila yanayowakabili Wapalestina, wanaopambana kwenye mazingira magumu yaliyoko Gaza.

Guterres hapo jana alitembelea kivuko cha mpakani cha Rafah kinachopakana na Gaza katikati ya miito inayoongezeka dhidi ya Israel ya kupunguza vizuizi na kufungua vivuko ili kuruhusu misaada kuingia Ukanda wa Gaza.